Friday, April 12, 2013

MIAKA 29 BAADA YA KIFO CHA EDWARD SOKOINE-HISTORIA,NUKUU NA PICHA

Hayati  Edward Moringe Sokoine


Edward Moringe Sokoine (1938 - 12 Aprili 1984) alikuwa Waziri Mkuu wa Tanzania kwa awamu mbili, tangu tarehe 13 Februari 1977 hadi 7 Novemba 1980, na tangu tarehe 24 Februari 1983 hadi kifo chake, alipofariki kutokana na ajali ya gari. 

Uongozi wake ulionekana kuwa wa mfano kwa jinsi alivyokuwa na uadilifu na kufuatilia utendaji kazi huku akikemea ulaji rushwa na ubadhirifu wa mali za umma. 

Sokoine alifariki kwa ajali ya gari wakati akitoka kwenye kikao cha bunge Dodoma kuelekea Dar es Salaam. Wengi wanashuku ajali hiyo kuwa ilipangwa, ingawa mpaka leo bado ni kiza kitupu.

Kifo chake kilileta majonzi makubwa kwa Watanzania wa kawaida ambao walikuwa wanamtarajia kuwatetea wanyonge na kuinua hali ya maisha yao. 
 
Mwili wa Edward Moringe Sokoine ulizikwa nyumbani kwao Monduli, mkoani Arusha.
Leo Tanzania inaazimisha miaka 29 tangu kufariki kwa ndugu Edward Moringe Sokoine (01/08/1938-12/04/1984)   Waziri Mkuu wa aina yake nchini Tanzania.Sokoine aliongoza katika kipindi ambacho nchi ilikuwa katika hali ngumu sana ya kiuchumi. 
Hayati Sokoine na Mwalimu Nyerere.
Zifuatazo ni nukuu muhimu za shujaa huyo kutoka katika Kitabu cha Edward Moringe Sokoine: Kiongozi wa Watu Aliyejitolea kilichoandikwa na Luteni Kanali Albert N. Kigadye mnamo mwaka 1984:


"Ole wake kiongozi mzembe na asiye na nidhamu nitakayemkuta: Kiongozi wa siasa hana usalama wa aina yoyote. Usalama wake ni kudra ya Mungu na Wananchi peke yake. Viongozi wazembe na wabadhirifu wahesabu siku zao. Labda tusiwajue. Hawa hatuna sababu ya kuwapa imani, kuwa tutawalinda kama vitendo vyao viovu" - Edward Moringe Sokoine, 26 Machi 1983

"Juu ya suala hili la mapato kutolingana na matumizi ni kwamba tungependa kupunguza uongezaji wa wataalam wasiohitajika katika Serikali na katika mashirika ya umma mpaka hapo hali yetu ya uchumi itakapokuwa katika hali nzuri" - Edward Moringe Sokoine, 23 Oktoba 1982
Gari la Hayati sokoine baada ya ajali.
"Serikali inasimamia bei, lakini Serikali yetu itakwenda mpaka itasimamia bei ya mhogo, dagaa na bei ya kila kitu? Haiwezekani, vitu vingine ni lazima vizalishwe kwa wingi ili bei yenyewe iweze kujirekebisha" - Edward Moringe Sokoine, 24 Septemba 1983

"Wajibu wa kila Mtanzania, kila familia na kila anayekula ni kujilisha mwenyewe. Si wajibu wa Taifa kumlisha mtu. Unaweza ukasaidiwa unapopatikana na janga. Lakini kama hakuna janga ni wajibu wa kila mtu aweze kujitosheleza kwa chakula na atoe ziada kwa Taifa" - Edward Moringe Sokoine, 4 Oktoba 1983

"Vijana leo wengi wana mali zaidi kuliko wazee waliofanya kazi miaka thelathini hadi arobaini. Lakini wanaitaka Serikali ndiyo iwaulize mali hiyo wameipata wapi. Hivi kwa nini mzazi asimuulize mwanae, 'mali hii umeipata wapi?'" - Edward Moringe Sokoine, 23 Oktoba 1983

"Katika nchi inayojali haki na usawa, majeshi hayana budi yawe ni chombo cha kulinda haki na maslahi ya walio wengi. Na kamwe hayaruhusiwi kuwa ni chombo cha wachache wenye kujali nafsi zao na kusahau maslahi ya walio wengi" - Edward Moringe Sokoine, 1Februari 1977

RAIS OMAR AL BASHIR KUZURU SUDAN KUSINI LEO.


JUBA-SUDAN KUSINI,Rais wa Sudan Omar Hassan Al Bashir anatarajiwa kuzuru nchini Sudan Kusini ijumaa hii na tayari maandalizi makubwa kwa ajili ya mapokezi yake yamekwishafanyika. Al Bashir anatarajiwa kukutana na mwenyeji wake Rais Salva Kiir na ziara hii itakuwa ni sehemu ya kumaliza mgogoro uliozuka baina ya pande hizo mbili.

Miongoni mwa mambo yatakayopewa kipaumbele katika mazungumzo ya viongozi hao ni suala la usalama ambalo limekuwa tete tangu nchi hizo zigawanyike mwezi Julai mwaka 2011.Muafaka kati ya viongozi hawa wawili unatajwa kuwa huenda ukawa chanzo cha kupunguza uhasama na hata kurahisisha utekelezaji wa makubaliano ya amani baina ya mataifa hayo.

Mpango wa Al Bashir kuzuru Juba uliwekwa wazi siku moja tu baada ya viongozi wa mataifa haya mawili ya Sudan kuafikiana kuanza upya biashara ya uzalishaji na usafirishaji wa mafuta.

Ziara ya Bashir mjini Juba itakuwa ni ya kwanza tangu kiongozi huyo alipohudhuria sherehe za uhuru julai 9 2011 kufuatia kura ya maoni iliyoamua Kusini ijitegemee baada ya miaka 22 ya machafuko.

CAG ABAINI UBADHILIFU MKUBWA SERIKALINI.


 

DODOMA-TANZANIA,
Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), ilitolewa jana ikiweka bayana madudu mbalimbali ya ubadhirifu mkubwa wa fedha za umma, udhaifu katika usimamizi wa mikataba na Serikali kushindwa kutoa fedha zilizoidhinishwa na Bunge kwa ajili ya miradi ya maendeleo.
Moja ya matatizo yaliyojitokeza ni Wizara ya Nishati na Madini kushindwa kukusanya nyongeza ya mrabaha wa madini baada ya kuongezwa kutoka asilimia tatu hadi nne.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kuwasilisha ripoti hiyo ya mwaka wa fedha unaoishia Juni 30, 2012, CAG Ludovick Utouh alisema pamoja na kuwapo mafanikio ya kimahesabu ukilinganisha na miaka iliyopita, bado kuna mambo ambayo yanatakiwa kufanyiwa kazi.
Alilishauri Bunge kuangalia upya suala la kuivunja Kamati ya Hesabu ya Mashirika ya Umma (POAC) na kuunganisha shughuli zake na Kamati ya Hesabu za Serikali Kuu (PAC) na mkakati wa ofisi kufanya ukaguzi wa misamaha ya kodi ambayo imeongezeka kuangalia uhalali wake.
Hata hivyo, Utouh alikataa katakata kuzungumzia deni la taifa ambalo pia limeongezeka akisema “amefanya hivyo makusudi”.
Bajeti na miradi ya maendeleo
Kwa mujibu wa CAG, imebainika kuwa kuna tatizo kubwa la Serikali kushindwa kutoa kwa halmashauri mbalimbali fedha za maendeleo kama zilivyopitishwa na Bunge.
Alisema Bunge lilipitisha vifungu vya fedha za maendeleo vyenye jumla ya Sh595,064,422,505 katika halmashauri 113, lakini fedha zilizopokewa ni Sh345,568,067,477 sawa na asilimia 42 tu, hivyo kufanya upungufu wa Sh249,496,355,027.
Licha ya fedha hizo kutokutolewa zote, kiwango kilichotolewa hakikutumika chote kutokana na kucheleweshwa. “Hadi mwishoni mwa mwaka, kulikuwa na baki ya fedha za miradi ya maendeleo kiasi cha Sh188,405,740,589 ambayo ni sawa na asilimia 55 ya fedha zilizotolewa na Serikali,” alisema Otouh na kuongeza: “Tunashauri bajeti iendane na shughuli zilizopangwa, kwa sasa utaratibu wa bajeti haujawa mzuri.”
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, hata fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo zinazotolewa kwa wabunge hazikutumika zote. Sh2,561,882,820 zilizotengwa kwa ajili ya sampuli ya majimbo 69 zilibaki.
“Sababu ya kutokutumika ni ama halmashauri hazina utaratibu maalumu wa kutumia fedha hizo au Serikali kutoa fedha hizo mwishoni mwa mwaka,” alisema.
Udhaifu katika usimamizi wa mikataba ya madini
Katika ripoti hiyo, CAG alisema Wizara ya Nishati na Madini ilishindwa kukusanya Dola za Marekani 12,634,354 (sawa na Sh19,709,593,191) zilizotokana na ongezeko la mirabaha ya madini, baada ya mabadiliko ya Sheria ya Madini.
Katika iliyokuwa Wizara ya Miundombinu, ukaguzi huo umebaini kuwa madeni yake ya mwaka 2010/11 yanayofikia Sh253 bilioni yamelipwa kwa kutumia fedha zilizoidhinishwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara mwaka uliofuata wa 2011/12.
Katika kipindi hicho, CAG alisema dhamana za Serikali za jumla ya Sh578.4 bilioni zilikuwa zimeisha muda wake na hivyo kuifanya Serikali ikiwa mdhamini kuwajibika kulipa deni hilo.
Vilevile, CAG ameona kuna kodi inayopotea kutoka sekta isiyo rasmi, hivyo kuishauri Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuwatumia vizuri makatibu kata kuwatambua walipakodi kama vile wamiliki wa kumbi za harusi na mikutano.(MWANANCHI)

OBAMA AIONYA KOREA KASKAZINI KUHUSU KUISHAMBULIA MAREKANI





WASHINGTON DC-MAREKANI, Rais wa Marekani Barack Hussein Obama hatimaye amefungua kinywa chake na kuishauri Korea Kaskazini kuachana na mpango wake wa kutaka kuingia kwenye vita katika kipindi hiki wakati kukiwa na uvumi kuwa serikali ya Pyongyang inataka kushambulia Washington kwa makombora. 

 Obama ametoa kauli hiyo akiwa katika Ikulu yake maarufu kwa jina la White House na kueleza hakuna mtu yeyote ambaye anapenda kushuhudia Dunia inaingia kwenye mgogoro utakaochangia vita.
Aidha Rais Obama amesisitiza umuhimu wa serikali ya Korea Kaskazini kuheshimu sheria na taratibu kama inavyofanyika kwa nchi nyingine duniani ili kuepusha migogoro zaidi.
Korea Kaskazini pia haikukwepa kidole cha lawama kutoka kwa Mawaziri wa Mambo ya Nje kutoka nchi tajiri zaidi duniani maarufu kama G8 walipokutana nchini Uingereza.
Akizungumza na waandishi wa habari pembezoni mwa mkutano huo Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza William Hague amesema endapo Pyongyang itafanya jaribio jingine la nyuklia hawatasita kuchukua hatua kali dhidi yake ikiwemo vikwazo vipya ambavyo vitaafikiwa katika baraza la usalama la umoja wa mataifa UNSC.
Hofu ya kutekelezwa kwa mashambulizi kutoka Korea Kaskazini kulenga Marekani na rafiki zake Japan na Korea Kusini imeendelea kuchanja mbuga licha ya makaripio mbalimbali kuzidi kutolewa kila uchao.