Tuesday, December 11, 2012

UPORAJI MSAFARA WA MAITI:WATUHUMIWA 25 WAKAMATWA

SINGIDA-TANZANIA, Watu 25 wametiwa mbaroni kwa tuhuma za utekaji gari dogo mali ya Chuo Kikuu cha Sokoine (Sua), kilichopo mkoani Morogoro na kupora abiria mamilioni ya fedha na vitu mbalimbali. Hata hivyo, Kamanda wa Polisi mkoani Singida, Linus Sinzumwa, alikataa kutaja majina ya watuhumiwa hao kwa maelezo kwamba kufanya hivyo kutaathiri mwenendo wa upelelezi. Watu hao wanatuhumiwa kuliteka gari dogo aina Toyota Land Cuiser SU 37012 lililokuwa na mwili wa mwanafunzi mwaka wa tatu wa Sua, Munchari Ryoba, uliokuwa ukisafirishwa kwenda Musoma mkoani Mara kwa mazishi.Gari hilo lilikuwa likiendeshwa na Kastus Mapulila.Baada ya majambazi kuliteka gari hilo, walilifungua  jeneza lenye mwili wa marehemu na kufanyia upekuzi.Tukio hilo la aina yake lilitokea usiku wa kuamkia Jumamosi iliyopita.Abiria waliokuwa wakiusindikiza mwili huo, waliporwa fedha taslim zaidi ya Sh. milioni 19, zikiwemo za rambirambi na vitu mbalimbali baada ya baadhi yao kushambuliwa kwa mapanga.Akieleza kukamatwa kwa watuhumiwa hao, Kamanda Sinzumwa alisema wengi wao ni wakazi wa kijiji cha Kisaki, kilichopo nje kidogo ya Manispaa ya Singida.Alisema msako huo unaoendelea pia umefanikisha kupatikana kwa baadhi ya mali zilizoporwa zikiwamo nguo, kamera, laptop na simu za viganjani.Alisema kukamatwa kwa vitu hivyo kumetokana na ushirikiano wa polisi na wananchi.Kamanda Sinzumwa alisema baada ya watuhumiwa hao kugawana fedha walizopora, walianza kulewa pombe hovyo huku wakidai hali za uchumi wao zimeimarika.Alisema baada ya kukamilisha kazi ya upelelezi, ikiwa pamoja na kuchuja kupata washiriki kamili wa tukio hilo, watafikishwa mahakamani ili sheria ichukue mkondo wake.

TAZARA YAANDAA TRENI MAALUM YA WATALII.


DAR ES SALAAM-TANZANIA. MAMLAKA ya Reli ya Tazara inaandaa treni maalumu ya kupeleka abiria katika hifadhi ya Selous mwisho wa mwezi huu ili kuwapa fursa abiria kubadilisha mazingira katika kusherehekea sikukuu za mwisho wa mwaka za Krismasi na Mwaka Mpya.
Safari hiyo itakayofanyika tarehe 29 Disemba mwaka huu itawawezesha abiria mbalimbali kujionea mandhari nzuri ya hifadhi ya Selous, kufurahi pamoja na familia zao pamoja na kujifunza mambo mbalimbali katika hifadhi hiyo.
Akizungumzia safari hiyo, Meneja Masoko wa Tazara Hemed Msangi alisema kuwa wamepokea maombi mengi kutoka kwa watu mbalimbali, hivyo wameona wawapatie abiria wao kitu wanachokitaka ili kukidhi matakwa yao.
“Safari hiyo ya siku moja itaanza saa 2 asubuhi na kurudi saa 1 jioni, kwa hiyo natoa rai kwa wananchi wote kutumia nafasi hiyo ili kusherehekea sikukuu kwa namna ya pekee sana,” alisema Msangi.
Msangi aliongeza kuwa abiria watachangia huduma hiyo ambapo watu wazima watalipia Sh70,000 na watoto Sh40,000 ikijumuisha nauli, chakula na vinywaji wawapo katika safari hiyo.(CHANZO:MWANANCHI)

TANESCO YAWEKEWA NGUMU KUPANDISHA GHARAMA ZA UMEME


WADAU mbalimbali wamepinga ombi la Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), kuongeza bei ya nishati hiyo kwa asilimia 155 ifikapo Januari mwakani.
Wadau hao wamesema   si wakati mwafaka sasa kwa Tanesco kupandisha bei ya umeme, kwani badonafasi kubwa ya kujikwamua katika mikwamo yake kwa  usimamizi bora wa rasilimali zake na kuboresha huduma kwa wateja.
Mambo mengine ambayo wadau hao waliyataja kuwa ni kikwazo kwa Tanesco kupandisha bei ya umeme ni rushwa ndani ya shirika hilo, mikataba mibovu, upotevu wa umeme kuanzia vyanzo vyake hadi kwa mteja na ukusanyaji mbovu wa madeni.
Wakizungumza jijini Dar es Salaam jana katika mkutano wa pamoja wa kupata maoni ya wadau kuhusu nia hiyo ya Tanesco, wadau hao walisema Tanesco haina sababu ya kupandisha bei ya umeme kwani bado inaweza kutumia rasilimali zake kujiendesha.
Tanesco imeomba ipandishe bei ya umeme kuanzia mwakani kutokana na sababu kadhaa ikiwamo ongezeko la gharama za uendeshaji na kukithiri kwa madeni ya shirika hilo la umma.

“Ongezeko la bei ya umeme ambalo linawezesha shirika kukidhi gharama za uendeshaji bila kupata faida ni asilimia 81.7 kutoka bei iliyoko sasa,” ilisema sehemu ya taarifa ya shirika hilo iliyowasilishwa kwenye mkutano huo na Kaimu Mkurugenzi wake Mkuu, Felchesmi Mramba.

Mramba alisema hadi Oktoba mwaka huu, Tanesco ilikuwa inadaiwa kiasi cha Dola za Marekani 250 milioni (Sh400 bilioni), madeni ambayo kimsingi yanachangia kurudisha nyuma maendeleo ya shirika. Hata hivyo, Mramba hakueleza madeni ambayo shirika hilo linawadai wateja wake ambayo yanaelezwa kuwa ni mengi yanayoweza kufidia kwa kiwango kikubwa pengo hilo.
Katika michango yao kwa nyakati tofauti, wadau hao walipinga maombi hayo ya Tanesco kuongeza bei ya umeme, badala yake wakalitaka shirika hilo kuongeza ufanisi katika utendaji wake ikiwamo kukusanya madeni kutoka kwa wateja na kutoa huduma bora kwao.
Mwakilishi wa Shirika la Ugavi wa Umeme Zanzibar (Zeco) Mohamed Suleiman Khatib, alisema hawakubaliani na ombi hilo la Tanesco akisema hata bei ya iliyopo sasa inawakandamiza wakazi na wawekezaji wa Zanzibar.
“Iwapo bei hizi zitaongezwa, basi wananchi wa Zanzibar watakuwa na maisha magumu kutokana na gharama za maisha kuongezeka. Pia wawekezaji watahama na kukimbilia Bara ambako kutakuwa na bei nafuu ya umeme.”
Khatib alieleza kuwa Zeco inatumia kati ya Mega Watti 55 hadi 60 sawa na asilimia 4 ya umeme wote nchini, lakini ripoti ya mshauri elekezi ilishindwa kumtambua kuwa ni mtumiaji mkubwa wa umeme, hali ambayo itaibebesha mzigo mkubwa
Makamu Mwenyekiti wa Barazala Ushauri la Ewura, Said Mohamed alisema hawakubaliani na kupandishwa kwa bei ya umeme kwa kiwango hicho ambacho Tanesco imekiomba.
Alisema hiyo inatokana na mshauri elekezi kutumia kiwango cha ongezeko la asilimia 40.29 kilichoanza mwaka huu kama msingi wa kutafuta bei mpya kwa miaka mitatu ijayo.(CHANZO:MWANANCHI).

JOHN DRAMANI NDIYE RAIS MPYA GHANA



ACCRA-GHANA,Tume ya uchaguzi nchini Ghana imemtangaza rais John Dramani Mahama mshindi wa uchaguzi wa urais  baada ya kupata ushindi wa asilimia 50 nukta 7 na kumshinda mpinzani wake Nana Akufo Addo aliyepata asilimia 47 nukta 7.

Ushindi wa Mahama wa asilimia 50 umeepusha zoezi hilo kuingia katika duru ya pili katika uchaguzi huo ambao asilimia 80 ya wapiga kura walijitokeza kupiga kura.
Licha ya tume hiyo ya uchaguzi kumtangaza Mahama kuwa mshindi, upinzani umepinga matokeo hayo na kusema kura ziliibiwa na zoezi hilo halikuwa huru na haki.
Upinzani umeongeza kuwa matokeo yaliyotangazwa hayaoneshi sauti ya watu wa Ghana na viongozi wa upinzani wa chama cha NPP watakutana siku ya Jumanne kujadili mustakabali wa uchaguzi huo.

Hali ya wasiwasi imeendelea kushuhudiwa jijini Accra huku kukiwa na hofu ya wafuasi wa upinzani kuzua fujo kupinga ushindi wa rais Mahama, wakati waangalizi kutoka Umoja wa Afrika na wale wa Kimataifa wakisema zoezi hilo lilikuwa huru na haki.

Akizungumza baada ya kutangazwa mshindi, rais Mahama ametoa wito kwa upinzani kukubali matokeo hayo aliyoyasema yanaonesha sauti ya wananchi wengi wa Ghana.
Mahama mwenye umri wa miaka 54 awali alihudumu kama Makamu wa rais kabla ya kuwa rais kwa muda, baada ya kufariki kwa rais John Atta Mills mwezi wa Saba mwaka huu.

Naye kiongozi wa upinzani Akufo Addo mwenye umri wa miaka 68 ni wakili wa maswala ya haki za binadamu na mtoto wa rais wa zamani wa nchi hiyo na itakumbukwa pia mwaka 2008 alishindwa kwa chini ya asilimia 1 katika uchaguzi huo.

Wafuasi wa rais Mahama wameendelea kusherehekea katika sehemu mbalimbali nchini humo  kuanzia usiku wa Jumapili  baada ya kiongozi wao kutangazwa mshindi.(CHANZO:GHANAWEB,RFI)