Tuesday, April 09, 2013

BUNGE LA BAJETI KUANZA LEO.

 
DODOMA-TANZANIA, Mkutano wa 11 wa Bunge la Bajeti unaanza leo mjini Dodoma, huku kukiwa na mabadiliko kadhaa ya taratibu za uendeshaji wa Bunge.
Taarifa iliyotolewa jana na Mkurugenzi Msaidizi wa Bunge (Habari), Deogratius Egidio ilieleza kuwa Bunge litaanza vikao vyake leo na kukamilika Juni 28, mwaka huu.
Kutokana na mabadiliko hayo, leo asubuhi Bunge litapokea Azimio la Marekebisho ya Kanuni za Bunge ambalo linatarajia kuwasilishwa na Naibu Spika, Job Ndugai.
Egidio alisema katika mkutano huo, mambo kadhaa yanaonekana kubadilishwa ikizingatiwa na utaratibu uliozoeleka tangu mwanzo wa kusoma kwanza Bajeti ya Serikali na baadaye kumalizia na bejti za wizara mbalimbali.
Aliyataja mabadiliko hayo kuwa ni utaratibu mzima jinsi ya uwasilishaji bajeti za wizara, kwa mwaka huu itaanza Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo itajadiliwa kwa siku tano. “Siku zote tumezoea kuona Bajeti ya Serikali ndiyo inayotangulia kuanza kuwasilisha bajeti yake, utaratibu huo umeonekana siyo mzuri kutokana na mapendekezo ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Fedha za Serikali (CAG), hivyo tunaanza na wizara zingine ili fedha wawe mwisho,” alisema Egidio.
Hata hivyo, taarifa za zilizopatika kutoka ndani zinadai kanuni nyingi zinatarajia kubadilishwa na kwamba, iwapo zitapitishwa zitapunguza meno ya Bunge dhidi ya kusimamia Serikali.
Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo, kesho itakuwa siku maalumu kwa Ofisi ya Waziri Mkuu kuwasilisha bajeti yake, ambayo itajumuisha wizara zote zilizo chini yake na inatarajia kujadiliwa kwa muda wa siku tano.
Mabadiliko mengine ni kuwasilishwa mezani kwa taarifa ya CAG kwa mwaka 2011/12 bila kujadiliwa na wabunge kama ilivyozoeleka.
Hata hivyo, Egidio hakueleza sababu za kutojadiliwa kwa ripoti hiyo, akisema hawezi kujua katika mikutano ya baadaye ya Bunge iwapo inaweza kupangiwa kujadiliwa. 

SERIKALI YARUDISHA VIBOKO MASHULENI


 



 DAR ES SALAAM-TANZANIA,
Serikali imesema itarudisha adhabu ya viboko kwa wanafunzi shuleni ili kujenga nidhamu na kujituma.Akizungumza Dar es Salaam jana wakati akizindua tovuti ya www.shledirect.co.tz inayowezesha wanafunzi kujisomea kwa njia ya mtandao, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo ilisema kuondolewa kwa adhabu ya viboko shuleni kumewafanya wanafunzi wengi kukosa nidhamu na wakati mwingine kujifanyia mambo kienyeji. “Wasipotandikwa mambo hayaendi, nilipokuwa mwalimu mkuu nilikuwa nawatandika kweli ndiyo maana shule yangu ilikuwa ikiongoza Mkoa wa Mbeya hivihivi hawaendi...” alisema huku akishangiliwa na wageni waalikwa.
"Wasipotandikwa mambo hayaendi, nilipokuwa mwalimu mkuu nilikuwa nawatandika kweli ndiyo maana shule yangu ilikuwa ikiongoza Mkoa wa Mbeya hivihivi hawaendi....". "
- Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo
Alisema watoto wa siku hizi wamekuwa wakitumia vibaya teknolojia ambayo ingeweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa katika masomo yao... “Tovuti kama hiyo ingewasaidia kwa masomo, lakini wao wanakimbilia kwenye facebook na mambo mengine yasiyofaa.” Aliyalaumu mashirika yasiyo ya kiserikali na haki za binadamu ambayo yamekuwa yakipigania kuondolewa kwa adhabu hiyo shuleni na kusababisha kushuka kwa nidhamu kwa kiasi kikubwa. Kadhalika alisema Serikali imepiga marufuku matumizi ya simu za mikononi kwa sababu baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakizitumia vibaya jambo ambalo linawarudisha nyuma kimasomo. “Simu tunazipiga marufuku, mwalimu akimkuta mwanafunzi na simu amnyang’anye ndizo zinatuharibia taifa letu.” Aliwapongeza wabunifu wa mtandao huo akisema ni wazalendo kwani wamekuwa msaada katika jitihada za Serikali kukuza elimu nchini. “Watu wanapiga kelele Mulugo na Kawambwa wajiuzulu, hata tukijiuzulu haitasaidia, bali kila Mtanzania atoe mchango wake katika elimu ili kuweza kuiendeleza.” Mwanzilishi wa tovuti hiyo, Faraja Nyalandu alisema itakuwa na manufaa kwa wanafunzi wa Tanzania kwani masomo yanayotolewa yanaandaliwa na walimu wazoefu wenye shahada hivyo wanafunzi watakapoitumia watapata manufaa makubwa. Maoni ya wadau Akizungumzia hatua hiyo ya Serikali, Waziri Kivuli wa Elimu Mafunzo ya Ufundi, Suzan Lyimo aliitaka iache kuangalia mambo madogo ambayo yanachangia kwa kiasi kidogo tu kudorora kwa elimu na kuacha mambo makubwa. “Kuna mambo makubwa zaidi yaliyotufikisha hapa tulipo, hii ni sawa na kushughulika na matawi na kuacha mizizi. Lazima tuangalie suala hili kwa upana zaidi, kuna ripoti nyingi na nzito hazijafanyiwa kazi mpaka sasa badala yake Serikali inaibuka na kuanza kutangaza vitu vidogo kama hivyo, wafanyie kazi kwanza ripoti ambazo zilitumia pesa nyingi za walipakodi kwani nyingi zina mapendekezo mazuri.” Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Mpwapwa, Rukonge Mwero alisema uzuri wa adhabu ya viboko ni kwamba haipotezi muda” Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Helen Kijo Bisimba alisema adhabu ya viboko haina maana katika kipindi hiki akisema wanafunzi wanapaswa kupewa adhabu ambazo zinawafundisha kama zile za kufanya usafi na kazi mbalimbali. “Viboko havifundishi zaidi ya kumpatia mwanafunzi maumivu na kusababisha aichukie shule. Waelimishwe kwa kuelekezwa lakini wakiendelea kukiuka, wapewe adhabu za kufanya kazi mbalimbali. Rais wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Gratian Mukoba alisema walimu hawapati faida yoyote kuwachapa au kutowachapa viboko wanafunzi.