Wednesday, December 19, 2012

MAJAMBAZI WAPORA MILIONI 150 DAR.



Majeruhi wa tukio la ujambazi lililotokea Kariakoo, Dar es Salaam wakiwa kwenye gari la Polisi wakipelekwa hospitali baada ya kunusurika vifo wakati watu wanaodhaniwa kuwa majambazi walipowafyatulia risasi na kupora fedha kutoka kwa mhasibu wa duka la Artan Ltd jana. (Picha na Evance Ng’ingo).
DAR ES SALAAM-TANZANIA,
MAJAMBAZI waliokuwa wamepanda pikipiki kwa mtindo maarufu wa mshikaki, wamevamia duka la Kampuni ya Artan Ltd na kupora Sh milioni 150, zilizokuwa zikitolewa dukani eneo la Kariakoo kwenda benki jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa za Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, uporaji huo ulifanyika pamoja na mauaji jana saa 4:45 asubuhi katika Mtaa wa Mahiwa na Livingstone, Kariakoo. Kampuni hiyo inajihusisha na uuzaji wa betri na magurudumu.
Akisimulia mkasa huo jana, Kamanda wa Polisi Kanda hiyo, Suleiman Kova alisema majambazi hao waliwavamia watumishi wa kampuni hiyo waliokuwa wakitoa fedha katika duka lao kuzipeleka benki.
Alisema wakati wameshazi toa nje na kuingiza katika buti la gari aina ya Toyota Corolla Saloon ambayo haijafahamika namba, majambazi hao watatu wakiwa katika pikipiki yenye namba T301 CCW, mmoja akiendesha na wawili wakiwa wamepanda kwa mtindo wa mshikaki, waliwazingira huku wakiwaamuru watumishi hao kushuka katika gari ili waondoke nalo.
“Baada ya hao watumishi kukataa, majambazi hawa waliamua kuwajeruhi kwa risasi katika sehemu mbalimbali za miili yao na kufanikiwa kuondoka na fedha hizo,” alisema Kova.
Kati ya majeruhi hao kwa mujibu wa Kova, mmoja ni ambaye ni mhasibu wa kampuni hiyo, Ahmed Issa (55) alifariki dunia kutokana na kuumizwa vibaya na risasi hiyo.
Kova alisema mwingine aliyeuawa ni mwendesha mkokoteni, Sadik Juma (38) ambaye alinyanyua jiwe ili awapige majambazi hao waliokuwa katika pikipiki wakiondoka na fedha hizo, lakini kabla ya kurusha, walimuwahi na kumpiga risasi ya kichwa.
Majeruhi mwingine aliyekuwa katika gari lililomiminiwa risasi wakati wa uporaji wa fedha hizo, Yussuf Issa ambaye ni mtoto wa mwenye mali, anaendelea na matibabu katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
Polisi waingilia kati
Kamanda Kova alisema mara baada ya kusikika kwa milio ya risasi, Polisi waliokuwa doria walifika eneo la tukio na kushirikiana na wananchi kuwasaka majambazi hao.
Alisema katika muda usiozidi robo saa, walimkamata mtuhumiwa wa kwanza aliyekimbilia kujificha katika Mtaa wa Kongo, Agustino Kayula ambaye kwa jina lingine anajulikana kama Frank Mwabinga (24).
“Huyu mtuhumiwa wa kwanza alikamatwa akiwa na bastola aina ya Browing ambayo ilikuwa imefutwa namba ikiwa na risasi moja na maganda matano ya risasi yalipatikana eneo la tukio na pikipiki hiyo,” alisema Kamanda Kova na kudai kuwa mtuhumiwa huyo amekiri kutumia silaha hiyo.
Kova alisema Polisi pia inamshikilia mlinzi wa duka hilo, Ally Said (42) kwa tuhuma za kula njama ili kufanikisha uporaji huo kutokana na kushindwa kupambana na majambazi hao licha ya kuwa na silaha. Mlinzi huo amedai kuwa bunduki yake haipigi risasi.
“Huyu mlinzi inaonekana kuna namna fulani amefanya maana alidai kuwa bunduki yake haipigi risasi, lakini tumeikagua ni nzima kabisa na inafanya kazi, licha ya hivyo majambazi waliwezaje kumuacha mtu ambaye ana silaha na kuwafuata watu wale moja kwa moja?” Alihoji Kova.
Muuza maji ndani
Kova alisema Polisi pia inawashikilia watuhumiwa wengine wawili mmoja aliyejulikana kwa jina moja la Mussa maarufu Alhaji, anayesukuma mkokoteni na Salum Athumani, muuza maji ambao waliletwa kwa msaada wa wananchi wakiwa wamejeruhiwa.
Alisema pamoja na kuwashikilia watu hao, lakini hawezi kuwaunganisha moja kwa moja mpaka uchunguzi utakapokamilika.
Maziko ya Sadik
Kamanda Kova alisema Sadik aliyeuawa wakati akijaribu kuwapiga jiwe majambazi hao, alikuwa akisaidia Polisi na kutokana na mchango wake, wanaahidi kushirikiana na familia kuhakikisha maziko yanafanyika salama.
Pia amewaonya wahalifu kuwa katika kuelekea Sikukuu za mwisho wa Mwaka mpya, polisi wamejipanga vizuri na wanaendelea na msako mkali.(CHANZO:HABARI LEO)

KESI YA MAUAJI YA KANUMBA-LULU ABADILISHIWA MASHITAKA




DAR ES SALAAM-TANZANIA,
Upande wa mashtaka hapo ulimbadilishia mashitaka msanii Elizabeth Michael, maarufu kama Lulu kutoka kuua kwa kukusudia hadi kuua kwa kutokukusudia katika tuhuma za kumuua msanii mwenzake, Steven Kanumba.Kwa  mabadiliko hayo Lulu ameepuka adhabu ya kunyongwa hadi kufa.  baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), kumbadilishia mashtaka, ambapo sasa anatuhumiwa kuua bila kukusudia, ingawa kama atapatikana na hatia , adhabu yake ni kifungo cha maisha au hata  kuachiwa huru.

Hii inatokana na kifungu cha 196 cha kanuni za adhabu ya kosa la kuua bila kukusudia, ambapo anayepatikana na hatia anaweza kuhukumiwa kifungo cha maisha, miaka kadhaa au kuachiwa huru.

Hata hivyo, baadhi ya wanasheria waliliambia gazeti hili kwamba uzoefu wa adhabu nyingi za kuua pasipo kukusudia zilizowahi kutolewa nchini, ni kati ya miaka 15 na wengine waliachiwa huru.

Lulu alifikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Aprili 11, mwaka huu akikabiliwa na tuhuma za kumuua Kanumba Aprili 7, 2012.

Alikuwa akidaiwa kutenda kosa hilo kinyume na kifungu cha 196 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA), shtaka ambalo mshtakiwa anayepatikana na hatia adhabu yake ni kunyongwa hadi kufa.

Hata hivyo, jana upande wa mashtaka ulieleza mahakamani kuwa kwa sasa imebadilisha mashtaka kutoka kuua kwa kukusudia na kuwa kuua bila kukusudia, kinyume cha kifungu cha 195 cha CP.

Mshtakiwa huyo alitarajiwa kusomewa mashtaka hayo mapya jana pamoja na maelezo yote ya kesi, ambapo angesomewa ushahidi wa mashahidi wote pamoja na vielelezo muhimu katika kesi hiyo.

Hata hivyo, hatua hiyo ilikwama kutokana na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Tumaini Kweka anayeiendesha kesi hiyo kutokuwapo mahakamani na badala yake aliwakilishwa na Wakili wa Serikali, Ofmedy Mtenga.

“Upelelezi wa shauri lako umeshakamilika na tungeweza kukusomea comital (maelezo ya kesi) leo, lakini kwa kuwa waendesha mashtaka hawapo basi tunaliahirisha mpaka tarehe nyingine.”, alisema Hakimu Mkazi Agustina Mmbando, anayesikiliza kesi hiyo katika hatua hiyo ya awali.

Taarifa hizo za kukamilika kwa ushahidi wa kesi hiyo zilipokewa kwa furaha na shangwe na msanii huyo, kiasi kwamba alishindwa kujizuia kuonyesha furaha yake.

Wakili wake Peter Kibatala aliiomba mahakama itoe ahirisho fupi hadi Ijumaa kwa ajili ya mshtakiwa kusomewa mashtaka haya mapya pamoja na maelezo ya awali.
Hakimu Mmbando alikubaliana na ombi hilo la Wakili Kibatala na akaahirisha kesi hiyo hadi Ijumaa.(CHANZO:MWANANCHI)