Tuesday, December 18, 2012

SIRI ZAIDI ZAFICHUKA MAUAJI YA POLISI NA RAIA KAGERA.

KAGERA-TANZANIA,
Mambo Mapya yameendelea kuibuka kufuatia madai kuwa vifo vya watu watatu wakiwamo polisi wawili wilayani Ngara mkoani Kagera vimetokana na askari hao kukusanya kwa nguvu mapato ya serikali.



Chanzo chetu kimeeleza kuwa Askari wa Usalama Barabarani wanapaswa kukusanya kiasi kisichopungua Shilingi milioni tatu kila mwezi na hatua hiyo imekuwa ikiwalazimu kwenda kukamata na kutoza faini mbalimbali katika maeneo hata yasiyo na usalama kwa maisha yao.

Kikizungumzia tukio la mauaji hayo, chanzo hicho kilidai kuwa kitendo cha polisi kwenda kukamata pikipiki iliyokuwa ikitengenezwa na mtuhumiwa huyo ambaye ni fundi jirani na gulio la kijiji hicho, hakikuzingatia taratibu.



Kwa msingi huo, chanzo hicho kimeeleza kwamba Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani ndiye anayepaswa kuwa mlalamikiwa wa kwanza katika mauaji hayo.

“Unajua ndugu mwandishi, haiwezekani kwenda kukamata pikipiki za watu hadi ndani ya gulio...mbaya zaidi unakwenda kukamata na pikipiki inayotengenezwa kwa fundi. Hakika hapa busara haikutumika hata kidogo, ndiyo maana mauaji kama haya yametokea,” kilidai chanzo hicho na kuongeza:
“Pamoja na kwamba Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani kuwa mlalamikiwa wa kwanza, kwa kiasi kikubwa serikali yetu nayo inachangia maana sisi askari wa usalama barabarani tunalazimika kuhakikisha tunafikisha kiwango cha fedha tunazopangiwa kwa kila mwezi na inapotokea tarehe zinaelekea ukingoni na makusanyo hayajafikia, matokeo yake ndiyo hayo.” 
Chanzo hicho kilipingana na taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Philip Kalangi, kwamba askari hao walikuwa kwenye operesheni maalum ya kukamata watu wasio na leseni na vyombo vya moto visivyofaa kwa matumizi ya usafirishaji wa abiria.




Kwa mujibu wa chanzo hicho, taarifa hiyo imechakachuliwa kwa lengo la kukwepesha ukweli wa jambo hilo kujulikana.

“Hakika hapakuwa na operesheni maalum kama Kamanda alivyodai isipokuwa ni utaratibu wetu wa kawaida kwenda kukusanya mapato ya serikali. Tatizo hapa ni kutaka kukwepesha ukweli wa mambo. Aidha, yeye mwenyewe au mkuu wa upelelezi wa wilaya ambaye atakuwa ameamua kuchakachua maelezo ili kuweka kinga ya kuonekana askari walikuwa kwenye makosa,” kilidai chanzo hicho.



Hata hivyo, Kamanda Kalangi alipoulizwa jana kuhusiana na taarifa hiyo, alisisitiza kuwa ilikuwa operesheni.

“Mimi ndiye Kamanda, kama kuna anyepinga taarifa nilizozitoa kamuulize huyo huyo,” alisema Kamanda Kalangi.



Alisema kutokana na mauaji hayo, Mkuu wa Polisi nchini, Said Mwema, ametuma kikosi maalum kutoka makao makuu ya polisi kinachotarajiwa kuingia mkoani Kagera jana. Hata hivyo, hadi jioni hakikuwa kimewasili. 

Alisema kikosi hicho kitaungana na wenzao wa mkoani Kagera kuchunguza kwa kina mauaji hayo askari hao wawili pamoja na raia mmoja.

Habari kutoka ndani ya Jeshi la Polisi zimedai kuwa askari hao wa Kikosi cha Usalama Barabarani, walikwenda katika kijiji na kata ya Mugoma kukamata vyombo vya usafiri na watu wanaoendesha bila leseni ili kuhakikisha wanafikisha kiwango cha makusanyo ya serikali waliyopangiwa kila mwezi.(CHANZO:IPP MEDIA)

JACOB ZUMA ASHINDA TENA UCHAGUZI ANC.


Jacob Zuma
Rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma amechaguliwa tena kuongoza chama tawala nchini humo cha ANC baada ya kupata kura 2.983 dhidi ya 3.977 ya kura zilizopigwa, ikiwa ni ishara ya kumfagilia njia ya kuelekea kwenye uchanguzi wa rais mwaka 2014.

Makamu wa rais wa Afrika Kusini Kgalema Motlenthe ambae awali alitangaza kuwania nafasi hiyo ameonekana kuanguka kisiasa baada ya kuchukuwa uamuzi huo na mwishowekujiondowa ili aendelee kukalia kwenye nafasi yake, ambayo sasa ameikosa.
Cyril Ramaphosa, mfanyabiashara maharufu nchini humo amechukuwa nafasi ya makamu mwenyekiti wa chama, na kumrithi Motlanthe. Cyril Ramaphosa, ni mtu wa karibu sana na rais Zuma na huenda akawa mrithi wa zuma katika chaguzi zijazo, iwapo Jacob Zuma ataamua kutowania muhula mwingine
Zuma alipewa nafasi ya kushinda uchaguzi huo, licha ya kukabiliwa na kashfa mbalimbali na suala la kukigawa chama hicho, kwani asilimia kubwa ya wajumbe wakuu wa chama hicho wanamuunga mkono.
Akiwahutubia wajumbe hao zaidi ya elfu nne siku ya jumapili iliopita, Jacob Zuma aliahidi kupiga vita suala la kukigawa chama na rushwa inayo kithiri ambapo mwenye amehusishwa kutumia vibaya mali ya umma kwa manufaa yake binafsi.
Mbali na hayo Zuma aliahidi pia kupambana na hali ya mgawanyiko katika chama na mzozo uliotikisa nchi hiyo kufuatia mgomo wa wafanyakazi wa migodini uliopelekea watu zaidi ya sitini kupoteza maisha.
Jacob Zuma ametetea utawala wake huku akiahidi kuboresha zaidi na kutia kipao mbele masuala ya elimu, kuopiga vita rushwa na kupiga vita wawindaji haramu wa mifugo ya vifaru.
Wajumbe wa chama cha ANC walianza kukutana tangu siku ya Jumapili iliopita huko Bloenfontein na kutamatisha kikao hicho baada ya kuwapata viongozi hao wapya.(CHANZO:RFI)